Addis Ababa.
Waswahili wanasema ‘Kupanda ngoma kushuka mchongoma’ na hicho ndicho kinachotarajiwa kutokea katika robo fainali za mashindano ya Kombe la Chalenji 2015 zinazotarajiwa kuanza leo kwenye Uwanja wa Addis Ababa, Ethiopia.
Michezo ya robo fainali inaangaliwa kiushindani zaidi kutokana na timu zilivyojiandaa na nyingine kukutana kwa mara ya pili kutoka katika kundi moja.
Katika timu nane zilizofuzu robo fainali ni mechi mbili zitazikutanisha timu zilizokutana katika hatua ya makundi ambazo ni vinara wa Kundi A ambao ni Tanzania Bara ‘Kilimanjaro Stars’ watarudiana na wenyeji Ethiopia, Wakati washindi wa pili wa Kundi C, Sudan Kusini watajiuliza kwa ndugu zao Sudan waliokuwa wote kundi moja.
Kocha wa Kilimanjaro Stars, Abdallah ‘King’ Kibadeni anautazama mchezo huo kuwa wenye changamoto kutokana na kucheza na wenyeji, ambao hushangiliwa kwa nguvu na mashabiki wao.
“Tulicheza nao Jumamosi jana (juzi) kule Awassa na kutoka sare 1-1, hivyo nahitaji kubadilisha mbinu ambazo naamini zitatupa mabao zaidi badala ya sare kama ile.
“Wenzetu wapo nyumbani na wanakuwa na nguvu ya mashabiki kwa nje ingawa hawaathiri mchezo kwa kiasi hicho, tutakachofanya ni kucheza soka letu na kuendelea kutengeneza nafasi,” alisema Kibadeni.
Sare iliyopata Ethiopia dhidi ya Tanzania Bara baada ya beki Salum Mbonde kujifunga ndiyo iliyowapa wenyeji hao nafasi ya kushinda kama washindani watatu bora.
Kocha wa Ethiopia, Yohannes Sahili alisema kucheza na timu ngumu kama Tanzania kunawafanya kuwa na tahadhari kubwa na hilo ni jambo la msingi kwao kama watahitaji kuendelea na mashindano.
Sahili alisema hakuna ubishi kuwa Tanzania Bara ni moja kati ya timu nzuri katika mashindano ya mwaka huu na hilo linathibitishwa na hatua ya makundi waliyomaliza bila kufungwa.
“Ni timu nzuri, wana mipango katika kila dakika wanayoitumia uwanjani, lakini tunahitaji pia kubadilika kama tunataka kushinda mchezo dhidi ya Tanzania.
“Kwa ujumla tunatakiwa kujiandaa vizuri, hatua ya sasa si kama makundi, ambayo unaweza kufungwa katika mchezo wa kwanza ukafuzu kwa mingine, najua utakuwa mchezo mgumu ila vijana wangu wako tayari kupambana,” alisema Sahili.
Kabla ya mchezo huo wa Stars dhidi ya Ethiopia, utatanguliwa na mechi kati ya Malawi na mabingwa wa kihistoria Uganda mchezo unaotegemewa kuwa na upinzani wa hali ya juu kutokana na ubora wa timu hizo mbili.
Michezo hiyo ya robo itahitimishwa kesho kwa Sudan Kusini kuvaana na ndugu zao wa Sudan katika mchezo wa mapema, kabla ya Rwanda kuishukia Kenya.
Nahodha wa Rwanda, Haruna Niyonzima alisema mipango yao tangu awali ni kutopoteza mchezo hata mmoja katika mashindano hayo, licha ya kufungwa na Tanzania Bara katika hatua ya makundi.
“Tulipanga tusifungwe, lakini tukazidiwa na Tanzania Bara ila tumejipanga upya na naamini tutashinda katika mchezo huu na kucheza fainali,” alisema kiungo huyo wa Yanga.
Musonye: Stars hii hapa aisee!
Katibu Mkuu wa Baraza la Vyama vya Michezo Afrika Mashariki na Kati (Cecafa), Nicholaus Musonye amekiri kushangazwa na kiwango kinachoonyeshwa na ‘Kilimanjaro Stars kwa sasa.
Akizungumza na gazeti hili, Musonye alisema hajawahi kuiona timu hiyo ikicheza kwa nafasi na kutulia ikipanga mashambulizi kama anavyoiona katika mashindano ya Cecafa ya mwaka huu, hasa juzi dhidi ya Ethiopia.
“Kiukweli hawa vijana wamebadilika, ni wapya au? wanapiga pasi nyingi na wanakaa na mpira, wanapanga mashambulizi ambayo yanaanzia nyuma na yanafika hadi upande wa pili wa adui.
“Nadhani ni moja ya timu nzuri katika mashindano ya msimu huu kwa upande wangu mimi, nimeona michezo yao miwili tu, lakini huu wa leo (dhidi ya Ethiopia) umenifanya nikubali kuwa wako katika kiwango kizuri hivi sasa,” alisema Musonye.
Comments
Post a Comment